Arsenal wako mbioni kukamilisha usajili wa wachezaji wawili wapya
Arsenal waongeza kasi kwenye dirisha la usajili
Klabu ya Arsenal inaonekana kuwa na shughuli pevu katika kipindi hiki cha dirisha la usajili, huku taarifa zikieleza kuwa mabingwa hao wa Premier League wako mbioni kukamilisha usajili wa wachezaji wawili wapya katika siku chache zijazo.
Baada ya kufanikiwa kuwanasa Piero Hincapie, Illan Meslier, na Christos Tzolis mapema msimu huu, kocha wa The Gunners anaendelea kuimarisha kikosi chake ili kukabiliana na changamoto mbalimbali, ikiwemo jeraha la beki wao muhimu, William Saliba.
Beki mpya anakuja kuziba pengo la Saliba
Taarifa kutoka kwa mwandishi Bruno Andrade zimebainisha kuwa Arsenal wako kwenye hatua za mwisho kumsajili beki wa kati ili kuziba nafasi ya Saliba ambaye anasumbuliwa na majeraha. Ingawa jina la mchezaji huyo bado halijawekwa wazi, inaelezwa kuwa dili hilo litakamilika haraka zaidi kuliko hata usajili wa Bruno Guimaraes.
“Sina jina hilo kwa sasa, kwa hiyo siwezi kusema ni taarifa ya kipekee. Lakini nikizungumza na mtu anayehusika na hali ya Bruno Guimaraes, Arsenal wako karibu kusaini beki wa kati ili kutatua, kwa muda, tatizo lililojitokeza kutokana na jeraha la Saliba,” alisema Andrade.
Kinda Mylo Bernard kutua Emirates
Kando na usajili wa wakubwa, Arsenal wanaendelea kuimarisha timu yao ya vijana (academy). Mwandishi Sam Dean amethibitisha kupitia mtandao wa X kuwa klabu hiyo inakaribia kumsajili kinda mwenye umri wa miaka 16, Mylo Bernard, akitokea Crystal Palace.
Hii ni sehemu ya mkakati wa klabu hiyo wa kusaka vipaji vitakavyoisaidia timu katika siku za usoni.
Bruno Guimaraes kutua Arsenal?
Kuhusu kiungo wa Newcastle United, Bruno Guimaraes, hali inazidi kuonyesha kuwa mchezaji huyo huenda akaondoka St James’ Park kufuatia kuondoka kwa kocha Eddie Howe. Inafahamika kuwa mawasiliano kati ya Arsenal na Newcastle yameshaanza.
Moja ya vyanzo vya habari vilivyozungumza na TEAMtalk vimesema:
“Kila mtu anaamini kuwa Bruno anaondoka sasa. Mambo yanaendelea vizuri na kuna hisia kuwa dili hili litatokea mapema badala ya kuchelewa.”
Arsenal bado wako kwenye mtifuano wa kusaka kiungo mchezeshaji na winga, huku majina kama Vinicius Junior na Bradley Barcola yakitajwa hapo awali. Mashabiki wa The Gunners sasa wanasubiri kuona ni nani atakayekuwa sura mpya ya sita ndani ya kikosi hicho kuelekea msimu mpya.