Emerse Fae amlipua Schweinsteiger kwa kauli ya 'ubaguzi'
Mgogoro wa kauli za Schweinsteiger
Kocha mkuu wa timu ya taifa ya Ivory Coast, Emerse Fae, ametoa shutuma nzito dhidi ya gwiji wa soka la Ujerumani, Bastian Schweinsteiger, akidai kuwa mchezaji huyo wa zamani alitoa maneno ya kibaguzi wakati akichambua mchezo wa Ivory Coast dhidi ya Ujerumani katika michuano ya Kombe la Dunia.
Schweinsteiger, ambaye aliwahi kuichezea Bayern Munich na Manchester United, alidai kuwa timu za Afrika hucheza soka la ‘kikabila’ (African football) ambalo mara nyingi ni la ‘ovyo’, ‘lisilo na mpangilio’, na ‘lisilotabirika’. Kauli hizi zimezua mjadala mkali na hasira miongoni mwa wadau wa soka barani Afrika.
Majibu ya Fae
Akizungumza baada ya kuiongoza Ivory Coast kufuzu hatua ya mtoano kwa mara ya kwanza katika historia yao kufuatia ushindi dhidi ya Curacao, Fae hakupepesa macho katika kulijadili suala hilo.
“Ni jambo la kusikitisha. Schweinsteiger alikuwa mchezaji mzuri sana; nimekuwa nikimkubali sana kama kiungo na jinsi alivyokuwa akiisoma michezo. Niliposikia maoni yake, nilipata fedheha kwake kama mwanadamu. Tunaweza kusema huu ni ubaguzi, kama tutaita mambo kwa majina yake sahihi.”
Fae aliongeza kuwa yeye na kikosi chake wataendelea kuonyesha uwanjani kuwa timu za Afrika si za kutegemea nguvu pekee, bali zina uwezo mkubwa wa kiufundi na kimbinu. Aidha, kocha huyo alidai kuwa huenda Schweinsteiger alitaka kuzua utata ili azungumziwe baada ya watu wengi kumsahau.
“Kuna wachezaji wengi wa zamani ambao huwa wachambuzi na wote wanatafuta njia za kuzua utata. Alikuwa nyota wa dunia na labda anahisi watu wameshamusahau,” alisema Fae.
Klopp akataa kuzungumzia suala hilo
Katika tukio lingine linaloonyesha namna suala hili lilivyo nyeti, kocha Jurgen Klopp, ambaye naye anafanya kazi ya uchambuzi katika michuano hiyo, alionekana kukataa kabisa kuingizwa kwenye mjadala huo.
Katika mahojiano na vyombo vya habari, Klopp alionekana kukasirishwa alipoulizwa maoni yake kuhusu kauli za Schweinsteiger. Alimaliza mahojiano hayo ghafla na kuondoka, akisisitiza kuwa hilo ni suala zito na hakuwa tayari kutoa maoni yoyote juu yake.
Baada ya kuona shinikizo la umma, Schweinsteiger alijaribu kupunguza makali ya maneno yake kwa kuandika katika mitandao ya kijamii, akipongeza uwezo wa kiufundi na nguvu walizoonyesha Ivory Coast uwanjani, ingawa tayari uharibifu ulikuwa umeshajitokeza.