Hatima ya Erling Haaland: Manchester City waweka msimamo kwa ajili ya 2027
Mustakabali wa staa wa Manchester City, Erling Haaland, umeanza kuteka vichwa vya habari huku kukiwa na taarifa za kuwepo kwa ‘makubaliano maalum’ kati ya mchezaji huyo na klabu yake kuelekea mwaka 2027.
Makubaliano ya siri 2027
Ingawa Haaland bado anaonyesha kiwango bora uwanjani, duru za soka zinaeleza kuwa kuna maelewano kati ya uongozi wa City na mchezaji huyo kwamba iwapo atahisi anahitaji changamoto mpya ifikapo mwaka 2027, klabu itakuwa tayari kuketi naye na kutathmini hali hiyo badala ya kufunga milango ya kuondoka.
Tangu ajiunge na City akitokea Borussia Dortmund mwaka 2022, Haaland amekuwa mashine ya magoli, akifunga mabao 168 katika mechi 204. Hata hivyo, kutokana na mabadiliko ya benchi la ufundi baada ya kuondoka kwa Pep Guardiola, uvumi kuhusu hatima yake umeanza kuongezeka.
Vigogo wa Hispania wajiandaa
Taarifa zinaeleza kuwa klabu kubwa za Hispania, Barcelona na Real Madrid, zinafuatilia kwa ukaribu hali hiyo. Vilabu vyote viwili vinaamini kuwa mwaka 2027 utakuwa ndio wakati muafaka wa kufungua milango ya mazungumzo na mshambuliaji huyo wa Norway.
Kwa sasa, Haaland anaendelea kuonyesha umuhimu wake ndani ya City, akiwa tayari amefunga mabao matano katika mechi tano za Ligi Kuu ya Uingereza na Ligi ya Mabingwa Ulaya msimu huu.
Ushindi wa kishujaa Old Trafford
Akizungumzia hali ya sasa klabuni, Haaland alionyesha furaha yake baada ya City kupata ushindi dhidi ya Manchester United, licha ya kucheza na wachezaji 10 baada ya Phil Foden kutolewa kwa kadi nyekundu.
“Ilikuwa ni hali ya tofauti kwetu kucheza tukiwa pungufu, lakini tumeonyesha utu na utayari wa kupambana. Enzo (Maresca) alitupa mpango mbadala na tukaufuata vyema. Tunahitaji wapambanaji uwanjani, na nadhani tuna kikosi chenye watu wanaopenda kupambana kweli,” alisema Haaland.
Aidha, mshambuliaji huyo hakusita kumsifu kipa wake, Gianluigi Donnarumma, kwa kiwango chake bora kilichosaidia timu hiyo kulinda ushindi wao.
“Donnarumma ni kama mbwa mwitu langoni, uwepo wake unampa kila mchezaji uwanjani hali ya kujiamini. Tuna bahati sana kuwa naye,” aliongeza Haaland.