Hofu yaikumba Man Utd kuhusu JJ Gabriel, dirisha la kuondoka lafunuka
Hofu ya kumpoteza ‘Kid Messi’
Manchester United imeingia kwenye taharuki kubwa baada ya kuibuka kwa taarifa kwamba nyota wao chipukizi, Joseph Junior Andreou Gabriel (JJ Gabriel), anataka kuondoka klabuni hapo. Kijana huyo mwenye miaka 15, ambaye alijipatia umaarufu mkubwa hivi karibuni baada ya kufunga hat-trick katika mechi yake ya kwanza kwenye UEFA Youth League dhidi ya FC Sabah U19, amekuwa gumzo kubwa kiasi cha kuitwa ‘Kid Messi’.
Hata hivyo, furaha hiyo ya mashabiki wa ‘Mashetani Wekundu’ imetoweka ghafla baada ya ripoti kubainisha kuwa Gabriel amewasilisha ombi rasmi la kuvunja usajili wake klabuni hapo ili kuwa mchezaji huru. Hatua hii imewaacha viongozi wa United wakiwa wamepigwa na butwaa, kwani kijana huyo amekuwa akiichezea klabu hiyo tangu akiwa na umri wa miaka 11.
Mwanya wa kisheria unaotishia mustakabali wake
Ingawa Manchester United imesisitiza kuwa haina mpango wa kumruhusu kijana huyo kuondoka kabla ya mkataba wake kuisha, kuna hofu kubwa kuhusu ‘mwanya’ wa kisheria ambao unaweza kumpa uhuru wa kuondoka mapema mwezi ujao.
Kwa mujibu wa taarifa kutoka Manchester Evening News, Gabriel anatarajiwa kutimiza umri wa miaka 16 tarehe 6 Oktoba. Kwa kuwa ana pasipoti ya Ireland, sheria za FIFA zinaweza kumruhusu kusajiliwa na klabu yoyote barani Ulaya pindi anapofikisha umri huo, jambo ambalo linaifanya United kuhisi haina uwezo mkubwa wa kuzuia safari yake ikiwa atataka kujiunga na miamba kama Real Madrid au Barcelona.
Klabu hiyo kwa sasa inachunguza sheria hizo kwa undani ili kuona kama kuna njia yoyote ya kumzuia, kwani hali hiyo inaonekana kuwa na utata mkubwa kisheria.
Ryan Giggs ametoa angalizo
Habari hizi zimekuja siku chache tu baada ya gwiji wa klabu hiyo, Ryan Giggs, kumsifu Gabriel na kusisitiza kuwa kijana huyo yuko mahali sahihi kwa ajili ya maendeleo yake ya soka.
Akizungumzia kipaji cha kijana huyo, Giggs alisema:
“Anahitaji kucheza mechi. Ni vigumu kama uko kwenye kikosi cha timu ya kwanza, lakini unahitaji kupata dakika za uwanjani. Hata hivyo, yuko katika klabu bora zaidi kwa sababu ya historia ya vijana wanaochipukia hapa na namna wanavyotunzwa. Ana watu wazuri wanaomzunguka ambao wamewahi kuichezea klabu hii.”
Kwa sasa, mashabiki wa United wanaendelea kusubiri kuona hatma ya kijana huyo ambaye alionekana kuwa ndiye tumaini jipya la akademi yao, huku uongozi ukijaribu kila liwezekanalo kuziba mwanya huo wa kisheria ili asiondoke.