Liverpool yamkataa Ibrahim Mbaye, imeelekeza nguvu zote kwa Yankuba Minteh
Mabadiliko ya mipango Anfield
Klabu ya Liverpool imefikia uamuzi mzito katika dirisha hili la usajili kwa kuachana na mpango wa kumsajili winga wa PSG, Ibrahim Mbaye, na badala yake kuelekeza nguvu zao zote kwa staa wa Brighton, Yankuba Minteh.
Hali hii inakuja wakati Liverpool ikiwa kwenye mchakato wa kukiboresha kikosi chao katika nafasi za pembeni kufuatia kuondoka kwa Mohamed Salah, huku kukiwa pia na uwezekano wa wachezaji wengine kama Cody Gakpo na Federico Chiesa kupata changamoto mpya kabla ya dirisha kufungwa.
Kwa nini wamemkataa Mbaye?
Ingawa Liverpool ilikuwa tayari imefikia makubaliano binafsi na Mbaye, bei ya kumsajili kijana huyo mwenye miaka 18 imekuwa kikwazo kikubwa. PSG wamepania kupata Euro milioni 70 kwa mchezaji huyo, kiasi ambacho Liverpool wanaona ni kikubwa sana kwa mchezaji ambaye hajacheza hata mechi 50 za kiwango cha juu katika soka la kulipwa.
Kama alivyoeleza mwandishi wa habari za michezo, Fabrice Hawkins kupitia mtandao wa X:
PSG wanataka Euro milioni 70 kwa Ibrahim Mbaye msimu huu. Hata kama bei hiyo ni ya kuanzia mazungumzo, inaonekana kuwakatisha tamaa klabu nyingi zinazomhitaji, ambazo zenyewe zinamuona mchezaji huyo wa Senegal kama mwenye thamani ya Euro milioni 50.
Kwa msingi huo, Liverpool wameamua kutozama katika gharama hizo, hali inayomfanya Mbaye kuonekana kama mchezaji ambaye hatatua Anfield msimu huu.
Yankuba Minteh ndiye chaguo la Liverpool
Habari njema kwa mashabiki wa Liverpool ni kwamba mtaalamu wa masuala ya usajili, Fabrizio Romano, amethibitisha kuwa klabu hiyo imefikia makubaliano binafsi na winga wa Gambia, Yankuba Minteh mwenye miaka 22.
Liverpool wameonyesha nia ya dhati kwa kupeleka ofa mbili mfululizo kwa Brighton, ya kwanza ikiwa ni pauni milioni 50 na ya pili pauni milioni 60. Inaaminika kuwa dili hilo linaweza kukamilika ikiwa Liverpool wataludi na ofa ya tatu inayokadiriwa kufika pauni milioni 66.
Nini kinafuata kwa Bradley Barcola?
Licha ya kuingia kwenye mazungumzo ya kumsajili Minteh, Romano amesisitiza kuwa mchezaji huyo hatakuja kama mbadala wa Bradley Barcola, bali wote wawili wanapangwa kusajiliwa.
Sio mbadala, bali ni nyongeza kwa Bradley Barcola, ambaye bado ni mlengwa mkuu wa klabu.
Kwa sasa, Liverpool wanaendelea na mazungumzo ya kila siku na PSG ili kufikia muafaka wa bei ya Barcola, huku matumaini yakiwa makubwa kuwa ada ya uhamisho inaweza kushuka kutoka pauni milioni 145 hadi kati ya pauni milioni 120 na 125, kutokana na PSG tayari kusajili washambuliaji wengine katika dirisha hili.