Manchester City waipiku Arsenal na Man Utd kwenye mbio za kumsajili Ayyoub Bouaddi
Man City wanavyocheza karata yao kwa Bouaddi
Klabu ya Manchester City inaonekana kupiga hatua kubwa mbele dhidi ya mahasimu wao wa Ligi Kuu England, Manchester United, Arsenal, na Chelsea katika kinyang’anyiro cha kumsajili kiungo machachari wa klabu ya Lille ya Ufaransa, Ayyoub Bouaddi.
Bouaddi, ambaye amekuwa akionyesha kiwango bora kwenye michuano ya Kombe la Dunia akiwa na timu ya taifa ya Morocco, amekuwa akifuatiliwa kwa karibu na vigogo wengi barani Ulaya. Mbali na klabu hizo za Uingereza, timu kama Real Madrid, Bayern Munich, na Paris Saint-Germain pia zimekuwa zikihusishwa na juhudi za kutaka huduma ya kijana huyo.
Ujanja wa Manchester City
Mchambuzi wa masuala ya soka, Ben Jacobs, amebainisha kuwa siri ya mafanikio ya Man City katika mazungumzo haya ni utayari wao wa kukubaliana na matakwa ya Lille. Wakati klabu nyingine zikihitaji mchezaji huyo kwa haraka, City wako tayari kusubiri.
“Bouaddi ni mchezaji ambaye City wanamtazama kwa ukaribu sana. Manchester United, Chelsea, na Arsenal wote wamemweka kwenye rada zao. Hii ni stori ya kusisimua ya usajili kwa sababu Lille wapo tayari kuuza, lakini wanapendelea dili la mwaka 2027. Man City wameonyesha utayari wa kujadili dili hili kwa njia ya mkopo au makubaliano ya awali, ili mchezaji aendelee kuwepo Lille kwa msimu mmoja zaidi,” alisema Jacobs kupitia talkSPORT.
Inaelezwa kuwa Lille wameweka bei ya Euro milioni 80 kwa timu zitakazokubali kumuacha mchezaji huyo abaki kwa mkopo, wakati wale wanaotaka kumsajili moja kwa moja wanatakiwa kulipa kiasi cha Euro milioni 100.
Alex Scott naye yumo kwenye rada
Mbali na Bouaddi, ripoti zinaonyesha kuwa Manchester United, City, na Arsenal pia wanatazamia kuimarisha safu zao za kiungo kwa kumnusa Alex Scott wa Bournemouth. Klabu ya Bournemouth imeweka bei ya takriban Euro milioni 80 kwa kiungo huyo.
Kwa upande wa Manchester United, wameonekana kuwa na orodha ndefu ya viungo wanaowafuatilia. Mbali na Scott, United wanatajwa kuwa na majina ya Aurelien Tchouaméni, Carlos Baleba, na hata Sandro Tonali ambaye pia anawindwa na Tottenham na Manchester City. Hata hivyo, kwa United, gharama za usajili zitakuwa kigezo kikubwa cha kama watasonga mbele na mipango hiyo au la.