Man Utd wajadili uwezekano wa kumsajili Alexander Sorloth kutoka Atletico Madrid
United watafuta mbadala wa Zirkzee
Manchester United wameingia katika harakati za kutafuta mshambuliaji mpya kabla ya dirisha la usajili kufungwa, kufuatia taarifa kuwa Joshua Zirkzee anaelekea kutimkia nchini Italia. Zirkzee anahusishwa na mpango wa kujiunga na Fiorentina kwa mkopo, huku kukiwa na chaguo la kumsajili moja kwa moja msimu ujao.
Hali hiyo imeilazimisha United kutathmini soko ili kuziba pengo lake, na jina la mshambuliaji wa Atletico Madrid, Alexander Sorloth, limejitokeza kama chaguo la kushtukiza. Ripoti zinaeleza kuwa wapatanishi wametoa ofa kwa klabu hiyo ya Old Trafford kumsajili mshambuliaji huyo mwenye kimo kirefu cha futi 6 na inchi 5.
Sorloth ni chaguo la busara?
Sorloth, raia wa Norway, anatajwa kuwa na sifa za kipekee zinazohitajika na kocha Michael Carrick katika eneo la ushambuliaji. Mchezaji huyo ana uzoefu wa soka la ushindani, akifanikiwa kufunga mabao 175 katika michezo 475 aliyocheza katika ngazi ya klabu kwenye maisha yake ya soka.
“Sorloth anafaa sana kwenye mfumo wa mshambuliaji namba 9 ambao United wanauhitaji ili kutoa changamoto kwa Benjamin Sesko,” inaeleza taarifa hiyo ya awali.
Inafahamika kuwa Sorloth yuko tayari kuondoka Atletico Madrid na angefurahia kurejea kwenye Ligi Kuu ya England (Premier League), ligi ambayo aliwahi kuichezea akiwa na Crystal Palace kati ya mwaka 2018 na 2020. Kwa upande wake, Atletico Madrid wako tayari kumuachia mshambuliaji huyo kwa bei sahihi, ingawa wanasisitiza kuwa lazima watafute mbadala wake kwanza.
Changamoto za usajili katika siku za mwisho
Sio Sorloth pekee anayehusishwa na United; klabu hiyo pia imetajwa kuwatazama Igor Matanovic wa Freiburg na nyota wa Crystal Palace, Jean-Philippe Mateta. Hata hivyo, hali ya United katika siku hizi za lala salama za dirisha la usajili inaonekana kuwa na mwelekeo wa kusaka wachezaji wa mkopo ili kuongeza nguvu bila kuingia kwenye gharama kubwa za muda mrefu.
Wachambuzi wa masuala ya klabu hiyo, Laurie Whitwell na Andy Mitten, wamebainisha kuwa uwezekano wa United kuongeza mshambuliaji mpya ni mkubwa. Mitten alisisitiza kuwa kikosi kinaonekana kuwa na upungufu mkubwa katika eneo la mbele, hivyo ni muhimu klabu kuchukua hatua haraka.
Wakati United wakijaribu kupiga hesabu zao, Atletico Madrid wenyewe wako bize kutafuta mbadala wa Sorloth, wakihusishwa na mipango ya kumsajili Gabriel Jesus kutoka Arsenal au Jonathan David wa Juventus. Kila kitu kinategemea nini kitatokea katika saa chache zijazo kabla ya dirisha la usajili kufungwa Jumanne.