Manchester United yatajwa kumtaka mshambuliaji mwenye uzoefu, Welbeck na Toney waingia kwenye rada
Mkakati wa United kuimarisha safu ya ushambuliaji
Klabu ya Manchester United inaendelea na mikakati yake ya kuboresha kikosi chake kuelekea msimu ujao, huku ripoti mpya zikionyesha kuwa klabu hiyo inatafuta mshambuliaji mwenye uzoefu. Lengo kuu ni kupata mchezaji atakayeweza kusaidiana na Benjamin Sesko, ambaye alionyesha kiwango bora katika miezi ya mwisho ya msimu uliopita.
Mchambuzi wa mambo ya soka, Ben Jacobs, amedokeza kuwa United wanahitaji mchezaji ambaye hana tu uwezo wa kufunga mabao, bali pia mwenye uwezo wa kuleta chachu ya uongozi ndani ya vyumba vya kubadilishia nguo. Sifa hizi ni muhimu kwa mchezaji atakayekubali jukumu la kusaidia timu hata kama hatacheza kila mchezo.
Welbeck na Toney kwenye rada
Katika orodha ya wachezaji wanaotazamwa na klabu hiyo, majina ya Danny Welbeck anayekipiga Brighton na Ivan Toney anayochezea Al-Ahli ya Saudi Arabia yamejitokeza kama chaguo za uzoefu.
Kuhusu uwezekano wa kurejea kwa Welbeck, Jacobs anasema:
“Tumewahi kuzungumza hapo awali kuhusu jinsi ambavyo ingekuwa jambo zuri kumrudisha mchezaji kama Danny Welbeck. Hakuna hatua kubwa iliyopigwa hadi sasa, lakini kama watatilia maanani suala hilo, mashabiki watapenda. Hata hivyo, sidhani kama Brighton wako tayari kumuuza.”
Kwa upande wa Ivan Toney, ambaye amekuwa na kiwango bora katika ligi ya Saudi Arabia akifunga mabao 32 katika michezo 32, changamoto kubwa inabaki kuwa mishahara yake na msimamo wake kuhusu maisha huko Uarabuni.
“Ivan Toney ni jina ambalo nimelitaja hapo awali, ambaye Manchester United wanamkubali. Mishahara inakuwa ni kikwazo kwa kiasi fulani kwa sababu anapata malipo mazuri kule Saudi Arabia. Tunasubiri kuona nini kitatokea baada ya Kombe la Dunia na kama yuko tayari kuondoka, licha ya uvumi mwingi kuwa anataka kurejea Ulaya,” aliongeza Jacobs.
Mahitaji mengine ya United
Mbali na safu ya ushambuliaji, Manchester United inaendelea na harakati za kuimarisha maeneo mengine ya timu. Inaripotiwa kuwa klabu hiyo imekamilisha mazungumzo ya kumsajili kiungo wa Atalanta, Ederson, ingawa bado hakujawa na uthibitisho rasmi.
Kipaumbele kingine kwa kocha na uongozi wa United katika dirisha hili la usajili ni kuimarisha nafasi ya beki wa kushoto (left-back) na winga wa kushoto. Vilevile, juhudi za kupata beki wa kati zinaendelea ili kuifanya timu kuwa imara zaidi katika michuano mbalimbali watakayoshiriki msimu ujao.