Paul Merson aponya kambi Chelsea kuhusu usajili wa Morgan Rogers wa £117m
Mgogoro wa mawazo kuhusu usajili wa Morgan Rogers
Usajili wa kiungo mshambuliaji Morgan Rogers kujiunga na Chelsea kutoka Aston Villa kwa ada ya pauni milioni 117 umezua mjadala mkali miongoni mwa wachambuzi wa soka nchini Uingereza. Wakati klabu hiyo ikikamilisha hatua za mwisho za usajili huo, gwiji wa Arsenal, Paul Merson, amekosoa hatua hiyo akidai mchezaji huyo hakuwa hitaji la dharura kwa The Blues.
Merson anaamini kuwa Chelsea imetumia fedha nyingi kupita kiasi kwa mchezaji anayocheza nafasi moja na nyota wao, Cole Palmer. Akizungumza na Sky Sports, Merson alisema:
“Ni pesa nyingi sana. Pesa za ajabu. Kumleta Morgan Rogers kwa £117m si kile ambacho Chelsea ilikihitaji. Wanao Cole Palmer! Wanacheza nafasi moja!”
Hofu ya Merson kuhusu uwezo wa Rogers
Mchambuzi huyo aliongeza kuwa shinikizo la ada hiyo ya uhamisho linaweza kumfanya mchezaji huyo kupata wakati mgumu, hasa ikizingatiwa kuwa Chelsea ni timu ambayo mara nyingi hukutana na wapinzani wanaocheza kwa kujilinda (parking the bus) kwenye Uwanja wa Stamford Bridge.
“Rogers atalazimika kubeba mzigo wa lebo hiyo ya bei. Atasema hakuna presha kwa sababu hakujilipia yeye mwenyewe, lakini huo ni uongo. Kila mtu atamuangalia pale mambo yatakapokuwa magumu,” alisema Merson.
Je, Enzo Fernandez yupo njiani kuondoka?
Kwa upande mwingine, nguli wa Chelsea, Joe Cole, ana mtazamo tofauti kuhusu ubora wa Rogers lakini anakubaliana na hali ngumu ya kifedha inayowakabili Chelsea. Cole anaamini usajili huu huenda ukawa mwisho wa Enzo Fernandez klabuni hapo ili kuweka uwiano wa hesabu za kifedha.
“Ninafuraha kwa sababu yeye (Rogers) ni mchezaji bora sana na amefanya vizuri. Lakini nadhani hiyo inaashiria Enzo huenda akawa mlangoni akitokea nje kwa sababu lazima uweke uwiano wa hesabu zako mahali fulani,” alieleza Cole kwenye kipindi cha The Rest Is Football.
Cole pia aliongeza kuwa licha ya Rogers kuwa kipaji kikubwa, bado anaamini Chelsea inahitaji mshambuliaji wa kati (centre-forward) ili kukamilisha kikosi chao kwa msimu ujao wa Ligi Kuu ya Uingereza.
Athari kwa Arsenal
Mbali na Chelsea, Merson pia alionyesha kusikitishwa na namna Arsenal ilivyokosa fursa ya kumsajili mchezaji huyo, huku akishangazwa na uamuzi wa Arsenal kumuuza Leandro Trossard. Merson anaamini kuwa Arsenal bado inahitaji kusajili mchezaji mwingine wa pembeni (winger) ili kuendelea kushindana kwenye ngazi ya juu kabisa ya soka barani Ulaya.
Wakati Chelsea ikisubiri kumtambulisha Rogers rasmi baada ya kufanyiwa vipimo vya afya, mashabiki wanasubiri kuona kama mchezaji huyo atathibitisha thamani yake uwanjani au kama maneno ya Merson yatageuka kuwa kweli.