Michael Owen: Man Utd walikosea kutomsajili Dominic Calvert-Lewin
United walipaswa kumpa nafasi Calvert-Lewin
Staa wa zamani wa Liverpool na Manchester United, Michael Owen, amedai kuwa miamba hiyo ya Old Trafford ilifanya makosa kutojaribu kumsajili mshambuliaji Dominic Calvert-Lewin wakati alipokuwa huru kujiunga na timu yoyote msimu uliopita.
Kwa sasa, Manchester United inawategemea Matheus Cunha na Benjamin Sesko katika safu ya ushambuliaji, lakini utendaji wao umezua maswali huku Sesko akionekana bado kuhitaji muda zaidi wa kukua. Owen anaamini kuwa Calvert-Lewin angekuwa chaguo bora na uwekezaji wa busara kwa timu hiyo.
Uwezo wake uwanjani
Calvert-Lewin, ambaye kwa sasa anang’ara akiwa na Leeds United, ameendelea kuonyesha ubora wake baada ya kuisaidia timu hiyo kuichapa Newcastle United mabao 4-1 hivi karibuni. Owen anasema kuwa licha ya changamoto za majeraha alizopitia huko nyuma, mshambuliaji huyo ni mchezaji mgumu sana kukabiliana naye anapokuwa fiti.
“Amekuwa akisumbuliwa na majeraha mara kwa mara, lakini akiwa fiti ni mchezaji mgumu sana kumzuia. Kwa ukosefu wa washambuliaji hodari tulionao katika miaka ya hivi karibuni, nilifikiri labda mojawapo ya timu kubwa kama Manchester United ingeweza kumpa nafasi kama mshambuliaji mbadala,” alisema Owen.
Leeds wamefanikiwa kumtuliza
Owen anaamini kuwa Leeds United wamefanya kazi nzuri ya kumsaidia mchezaji huyo kurejea kwenye ubora wake na kumfanya kuwa na utimamu wa mwili ambao hapo awali ulikuwa mtihani mkubwa kwake.
“Lazima kuna kitu wanakifanya kule Leeds kumweka katika mstari sahihi na kumfanya awe fiti. Anacheza karibu kila mchezo, jambo ambalo hakuwa akilifanya hapo awali. Amekuwa na miaka kadhaa migumu, lakini sasa yupo katika ulimwengu mwingine ambapo anacheza mara kwa mara na anaonekana kuwa tishio,” aliongeza Owen.
Hali ya Benjamin Sesko
Kwa upande mwingine, legendari Teddy Sheringham ametoa maoni yake kuhusu mshambuliaji kijana wa United, Benjamin Sesko. Sheringham anaamini kuwa Sesko ana kipaji kikubwa lakini jukumu la kucheza kama namba 9 pekee yake katika soka la kisasa si kazi ndogo.
“Kucheza kama mshambuliaji pekee ni kazi ngumu sana. Inahitaji aina fulani ya mchezaji kuongoza safu ya ushambuliaji, kutunza mpira, kukimbia nafasi na kufunga mabao. Sesko atakuwa mchezaji mzuri, lakini bado anahitaji uzoefu na kujiamini zaidi ili kufika kilele cha ubora,” alieleza Sheringham.