Fabrizio Romano aibua mapya kuhusu mustakabali wa Mohamed Salah na Besiktas
Uvumi wa Salah kujiunga na Besiktas wakanushwa
Mustakabali wa nyota wa Liverpool, Mohamed Salah, umezidi kutawala vichwa vya habari baada ya kuibuka kwa taarifa zinazodai kuwa mshambuliaji huyo amefikia makubaliano ya kujiunga na klabu ya Besiktas ya Uturuki. Hata hivyo, klabu hiyo ya Uturuki imejitokeza na kukanusha vikali madai hayo.
Taarifa za awali zilizotolewa na mwandishi wa habari nchini Uturuki, Yağız Saffunçuoğlu, zilidai kuwa Besiktas imefikia mwafaka na Salah, huku ikidaiwa kuwa wakala wa mchezaji huyo alikuwa jijini Istanbul kwa ajili ya mazungumzo. Hata hivyo, Besiktas imetoa taarifa rasmi ikieleza kuwa taarifa hizo ni za uzushi.
Besiktas yatoa tamko rasmi
Katika taarifa iliyotolewa na Besiktas, klabu hiyo imekosoa vikali taarifa hizo za vyombo vya habari, ikisisitiza kuwa hazina ukweli wowote na ni uvumbuzi wa mwandishi husika.
“Yaliyomo kwenye taarifa za mwandishi Yağız Saffunçuoğlu kuhusu mchakato wa usajili wa klabu yetu ni ya kubuni kabisa. Mtu huyo amekuwa akisambaza ripoti zisizo na ukweli kwa muda mrefu, jambo linalopotosha umma,” ilisema sehemu ya taarifa hiyo ya klabu.
Besiktas imeongeza kuwa taarifa zozote rasmi kuhusu usajili zitawasilishwa kupitia njia zao rasmi za mawasiliano, na kuwataka mashabiki kupuuza tetesi zinazoenezwa mitandaoni.
Ufafanuzi wa Fabrizio Romano
Licha ya Besiktas kukanusha, mtaalamu wa masuala ya usajili barani Ulaya, Fabrizio Romano, ametoa ufafanuzi wake akisisitiza kuwa ni kweli Besiktas imemuwekea ofa Salah, ingawa hakuna makubaliano yaliyokamilika.
Romano alieleza kupitia chaneli yake ya YouTube kuwa hatua ya Besiktas kukanusha ni sehemu ya utaratibu wa kulinda usiri wa mazungumzo hadi makubaliano ya kina yatakapofikiwa.
“Kwa nini Besiktas imekanusha uvumi huo kupitia taarifa rasmi? Ni kwa sababu dili la Salah halijakamilika. Kabla ya makubaliano kufikiwa, klabu lazima ziwe makini. Besiktas wanamfuatilia Salah na walifanya ofa, lakini tunapaswa kusubiri kabla ya kuthibitisha chochote,” alisema Romano.
Salah bado anapima chaguzi zake
Mohamed Salah, ambaye Liverpool ilithibitisha mapema Machi kuwa ataondoka mwishoni mwa msimu huu baada ya miaka mingi ya mafanikio Anfield, bado hajafanya uamuzi wa mwisho kuhusu wapi atakapoelekea.
Mbali na Besiktas, mshambuliaji huyo wa kimataifa wa Misri anahusishwa na ofa kutoka nchi za Saudi Arabia, vilabu vya Major League Soccer (MLS), pamoja na ligi mbalimbali barani Ulaya. Wakala wake, Ramy Abbas Issa, kupitia mtandao wa X, ameweka wazi kuwa bado hajui Salah atachezea wapi msimu ujao, ingawa uamuzi huenda ukajulikana hivi karibuni.