Pape Matar Sarr aelekea Juventus, dili la Richarlison latikisa dili la Ndiaye
Pape Matar Sarr aelekea Juventus
Klabu ya Tottenham Hotspur imefikia makubaliano ya kumruhusu kiungo wao, Pape Matar Sarr, kujiunga na mabingwa wa Italia, Juventus. Mtaalamu wa masuala ya usajili, Fabrizio Romano, amethibitisha kukamilika kwa dili hilo kwa kutumia kauli yake maarufu ya “here we go”.
Sarr anatarajiwa kujiunga na Juventus kwa mkopo wa awali, huku kukiwa na kipengele cha kumlazimisha Juventus kumnunua jumla mchezaji huyo kulingana na vigezo maalum vilivyowekwa. Inaripotiwa kuwa dili hilo lote lina thamani ya Euro milioni 30.
Uhamisho huu unakuja baada ya Juventus kuhitaji haraka kuimarisha eneo lao la kiungo kufuatia changamoto za majeraha kwa wachezaji wao na kushindwa kupata saini za malengo mengine. Sarr mwenyewe alikuwa na shauku kubwa ya kujiunga na miamba hiyo ya Turin.
Richarlison kizuizi cha usajili wa Iliman Ndiaye
Wakati Sarr akiondoka, Tottenham bado inaendelea na pilikapilika za kutaka kumsajili Iliman Ndiaye kutoka Everton. Hata hivyo, Romano amebainisha kuwa dili hilo linashikiliwa na uamuzi wa mshambuliaji Richarlison.
Tottenham tayari imeshafikia makubaliano binafsi na Ndiaye, lakini mpango huo unahitaji Richarlison akubali kuelekea Everton ili mambo yaweze kwenda sawa.
“Leo Jumatatu, tutapata picha kamili ya nini kinaendelea na Iliman Ndiaye. Yeye ndiye lengo namba moja la Tottenham. Wameshafikiwa muafaka na mchezaji pamoja na mawakala wake. Tunangoja tu kuona kama Richarlison ataikubali ofa ya kwenda Everton, jambo ambalo litafungua mlango wa Ndiaye kutua Tottenham,” alisema Romano.
Ikiwa Richarlison atakataa mpango huo, mustakabali wa Ndiaye unaweza kubadilika na klabu nyingine zinazomtolea macho kama Manchester City zinaweza kuingilia kati. Saa chache zijazo zitakuwa muhimu sana katika dirisha hili la usajili kwa Spurs.