Thomas Tuchel kusalia England, siri za mkataba wake na Pep Guardiola zafichuka
Mustakabali wa Tuchel ndani ya England
Baada ya England kutolewa katika hatua ya nusu fainali ya Kombe la Dunia dhidi ya Argentina, mjadala mkubwa umeibuka kuhusu hatma ya kocha Thomas Tuchel. Licha ya mashabiki wengi kuonesha kutoridhishwa na matokeo hayo, ripoti za hivi punde zinaeleza kuwa Chama cha Soka cha England (FA) bado kina imani kubwa na kocha huyo raia wa Ujerumani.
Taarifa iliyotolewa na The Athletic imeweka wazi kuwa, licha ya shinikizo la umma, FA haikusudii kuachana na Tuchel kwa sasa. Inafahamika kuwa pande zote mbili zimekubaliana kuendelea na ushirikiano wao baada ya tathmini ya kina kuhusu mchezo huo dhidi ya Argentina.
Pep Guardiola alikuwa chaguo la kwanza
Jambo moja la kushangaza lililofichuka kwenye ripoti hiyo ni juhudi za FA kumsaka Pep Guardiola kabla ya kumpata Tuchel. Inasemekana kuwa kulikuwa na makubaliano ya mdomo kati ya pande hizo mbili kabla ya kocha huyo wa Manchester City kubadili mawazo na kuamua kuongeza mkataba wake ndani ya klabu hiyo ya Etihad.
“Lengo la kwanza lilikuwa Pep Guardiola, ambaye kulikuwa na makubaliano ya mdomo kabla hajaamua kusalia Manchester City. Hiyo ndiyo iliyoifanya FA kumgeukia Tuchel, ambaye pia ni mshindi wa Ligi ya Mabingwa Ulaya,” ilieleza ripoti hiyo.
Vipengele maalum vya mkataba (Exit Clauses)
Ripoti hiyo pia imeweka wazi siri zilizopo kwenye mkataba wa Tuchel, zikielezea vipengele vya kuachana na ajira hiyo (exit clauses). Vipengele hivi vilikuwa vimewekwa ili kulinda maslahi ya pande zote mbili endapo matokeo yangekuwa mabaya katika hatua za awali za michuano.
Kulikuwa na makubaliano kwamba kama England ingengolewa kwenye hatua ya makundi, 32-bora, au 16-bora, ingekuwa rahisi kwa pande hizo mbili kuketi na kuvunja mkataba kwa makubaliano. Katika hali hiyo, FA ingemlipa Tuchel fidia, au kama Tuchel angepata nafasi nyingine kubwa, yeye angeweza kuondoka huku FA ikipata fidia.
Hata hivyo, ilibainika kuwa kulitolewa msamaha maalum kwa hatua ya 16-bora baada ya kuonekana kuwa England ilikuwa na ratiba ngumu ya kukabiliana na Mexico katika uwanja wa Azteca.
Safari inaendelea
Ingawa wengi wamemnyooshea kidole Tuchel kwa mbinu zake baada ya England kuongoza dhidi ya Argentina na kisha kurudi nyuma na kuruhusu mabao mawili, FA inaonekana kutazama mbali zaidi. Kwa sasa, Tuchel anaendelea na kibarua chake cha kukijenga upya kikosi hicho cha ‘Three Lions’ kwa ajili ya changamoto zijazo.