Jurgen Klopp aondoka kwenye mahojiano baada ya kuulizwa kuhusu utata wa Bastian Schweinsteiger
Klopp akataa kuzungumzia suala la kibaguzi
Kocha wa zamani wa Liverpool, Jurgen Klopp, ameonesha kukerwa na maswali ya waandishi wa habari baada ya kuamua kuondoka ghafla kwenye mahojiano aliyokuwa anayafanya nchini Marekani. Tukio hilo lilitokea wakati Klopp alipoulizwa maoni yake kuhusu utata unaomkabili kiungo wa zamani wa Bayern Munich na Manchester United, Bastian Schweinsteiger.
Sakata hilo lilianza baada ya Schweinsteiger kutoa maoni yake wakati akichambua mchezo kati ya Ujerumani na Ivory Coast. Katika uchambuzi wake, Schweinsteiger alidai kuwa Ivory Coast wanacheza soka la “Kiafrika” ambalo alilielezea kuwa ni “la aina yake, la mwitu kidogo, na lisilo na mpangilio mzuri wa kiufundi.” Matamshi hayo yameibua mjadala mkali nchini Ujerumani, huku wengi wakiona kuwa ni ya kibaguzi.
Majibu ya Klopp yashangaza wengi
Klopp, ambaye kwa sasa anafanya kazi kama mchambuzi wa soka katika kituo cha Magenta TV, hakuwa tayari kuingia kwenye mtego wa kujadili suala hilo. Alipoulizwa na mwandishi wa habari wa Ujerumani, Klopp alionekana kukerwa na kusisitiza kuwa hayuko tayari kujadili mada hiyo.
“Na sasa unataka kuendeleza mada hii. Hapana, hapana, sina nafasi ya kujibu swali hili. Hili ni suala zito. Sijui hata nini ni sahihi kukisema. Kwa watu wa Afrika ni jambo moja, kwa watu wengine ni lingine, na mimi siko hapa kwa ajili hiyo. Namshukuru Mungu nilidhani hakuna atakayeniuliza kuhusu hili. Umetafuta muda na cha kushangaza wewe ni Mjerumani. Hilo limenishangaza sana. Asante sana,” alisema Klopp kabla ya kuondoka eneo hilo.
Je, Schweinsteiger ana nia mbaya?
Baada ya kuona matamshi yake yameleta taharuki, Schweinsteiger alitumia mitandao ya kijamii kufafanua msimamo wake baada ya ushindi wa Ujerumani wa mabao 2-1. Aliandika kuwa Ivory Coast walikuwa wapinzani wagumu na walionyesha ubora wa kiufundi na nguvu za kimwili.
Kwa upande wake, mwandishi wa habari wa michezo nchini Ujerumani, Phillip Awounou, alieleza katika makala yake kupitia jarida la Spiegel kuwa nyuma ya maneno kama “mwitu” na “lisilotabirika” kuna mifumo ya kibaguzi iliyokita mizizi tangu enzi za ukoloni. Hata hivyo, Awounou alisisitiza kuwa matamshi hayo hayamaanishi kwamba Schweinsteiger ni mbaguzi.
“Hiyo siyo kweli. Bila kujali maneno yake yenye utata, Schweinsteiger si mbaguzi na hatakiwi kuitwa hivyo,” alihitimisha Awounou.